Friday, October 11, 2013

BAADA YA WAZIRI WA UJENZI KUITEKELEZA SHERIA WAZIRI MKUU ATENGUA MAAMUZI YAKE.

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ametengua maamuzi yaliyofanywa na Waziri wa Ujenzi Dk. John Magufuli ya kuongeza tozo ya asilimia tano kwa wasafirishaji wa malori na mabasi kwa uzito unaozidi.

Agizo la kurudisha asilimia hiyo ya tozo ilitangazwa na Dk. Magufuri Oktoba Mosi mwaka huu na kusababisha manung’uniko kutoka kwa wasafirishaji huku wa malori wakigoma kuanzia juzi.

Waziri Mkuu aliitangaza uamuzi huo jana jijini Dar es Salaam mbele ya waandishi wa habari.

Pinda alisema baada ya kukutana na wadau wa usafirishaji nchini na kusikiliza maelezo yao, alibaini masuala kadhaa ambayo aliona ni vyema yakaangaliwa upya ili sekta hiyo isizorote na baada ya hapo alikutana na Baraza la Mawaziri na kukubaliana mambo kadhaa.

“Kwa kuwa kuna mvutano kati ya Wizara ya Ujenzi na wasafirishaji wa malori na mabasi kuhusu kanuni ya 7 (3) ya Sheria ya Usafirishaji ya mwaka 1973,  kwamba haitekelezeki kirahisi,  nimeiagiza  wizara  ikutane na wadau mbalimbali kwa ajili ya kupitia kila jambo linalohitajika,” alisema.

Wadau hao ni Wizara ya Ujenzi, Wizara ya Uchukuzi, Wizara ya Viwanda na Biashara, Chama Cha Wamiliki wa Mabasi (Taboa), Chama cha Wamiliki wa Malori (Tatoa), Ofisi ya Waziri Mkuu  na ya  Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG).

Pinda alisema: “Tumewapa mwezi mmoja wa kulishughulikia suala hili kwani ni jambo linalohitaji uamuzi mzuri, na tunategemea kuwa watakuja na majibu mazuri kwa muda tuliowapa.”

Aliongeza: “Nalisema hili kwa kuwa sisi kama nchi tunapaswa kuliangalia vizuri, na ni lazima tuziangalie barabara zetu tunazozijenga kwa gharama kubwa.”

 

Pinda alisema kutakuwa na uwezekano wa kuwapo kwa msongamano wa mabasi na malori kwenye mizani na serikali imeshauri kuwa mizani ya Kibaha itumike kwa ajili ya mabasi tu na ile ya Mikese kwa ajili ya malori, na kwamba  njia za Tanga, Moshi na Arusha zitalazimika kutafutiwa utaratibu mwingine wa mizani.

Pia aliitaka timu hiyo, wakati wa majadiliano yao, kuangalia suala la watumishi ambao siyo waaminifu kwenye mizani.

“Wakati naongea na wadau hao mmoja aliniambia kuwa bado kuna matatizo kwenye mizani kwani alisema gari lake lilizuiliwa kwa kuwa lilipatikana na kosa, lakini  alitoa rushwa na akaachiwa, kwa hiyo tatizo hilo bado lipo na linapaswa kuangaliwa,” alisisitiza.

Alisema jambo jingine linalopaswa kuangaliwa ni hali ya mizani, kwani kuna malalamiko kuhusu utofauti wa uzito katika baadhi ya mizani na kwamba amehakikishiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) kwamba wapo mbioni kufunga mizani nyingine ambazo ni za kisasa zaidi.

Pia alitaka kuwapo kwa mawasiliano kati ya taasisi za serikali hasa pale linapotokea jambo linaloigusa sekta nyingine ili wapate kuzungumza  na kwamba katika hali ya sasa ni vyema ukawapo utaratibu wa kuwashirikisha wadau katika kila sekta hizo ili kuleta uelewano.

Kuhusu chimbuko la mgogoro, Pinda alisema kulikuwa na mambo mawili, ambayo ni barua ya aliyekuwa Waziri wa Ujenzi wa wakati huo, Basil Mramba, ambayo aliiandika mwaka 2006 ya kutoa msamaha kwa tozo kwa uzito wa magari uliozidi ndani ya asilimia tano ya uzito unaokubaliwa kisheria.

“2006 Mramba alipata taarifa kuwa mizani ina matatizo na akaona aweke utaratibu wa ahueni kidogo, kwa hiyo barua hiyo ikawa inatumika isivyo sawa kwani kila aliyezidisha uzito alitumia mwanya huo ili asilipishwe na hivyo kuchangia kutokuwapo kwa uadilifu,” alisema.

Alitaja jambo lingine kuwa ni la kisheria, na kwamba Waziri Magufuli aliamua kutumia sheria kwa kuwa mwongozo wa Mramba haukuwa wa kisheria pamoja na kwamba uamuzi wake ulikuwa na nia njema.


No comments:

Post a Comment