Friday, August 16, 2013

BAADA YA ZIARA YA MWAKYEMBE JAMAA HUYU ADAKWA NA MADAWA YA KULEVYA.

Baada ya Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe kufanya ziara ya kushutukiza katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere (JNIA)baada ya kuwa uchochoro wa kupitishia dawa za kulevya, umeanza kuzaa matunda baada ya mtu mmoja kukamatwa akiwa na pipi 86 na misokoto 34 ya bangi.

Kukamatwa kwa dawa hizo kumekuja saa kadhaa baada ya Dk. Mwakyembe, kufanya ziara ya kushtukiza katika uwanja huo na kubaini kuwa JNIA kufanywa uchochoro wa kupitishia dawa za kulevya tatizo siyo ukosefu wa vifaa bali ni wafanyakazi wenyewe waliopewa dhamana ya kuusimamia.

Waziri Mwakyembe alifanya ziara hiyo juzi alfajiri na mtuhumiwa wa kusafirisha dawa alikamatwa siku hiyo hiyo saa 2:15 usiku.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Dk. Mwakyembe alimtaja aliyekamatwa kuwa ni Leonard Jeremiah Monyo (Pichani juu) ambaye alikamatwa juzi katika uwanja huo akisafirisha dawa za kulevya aina ya Heroen kwenda Italia kupitia Zurich, Uswisi.

Alisema mtu huyo ambaye ni raia wa Tanzania, alikamatwa katika uwanja huo baada ya kufanyiwa ukaguzi na wanawake wawili ambao ni wafanyakazi wa JNIA kubaini kuwa alikuwa amezificha dawa hizo katika begi lake.

Naye Kamanda wa Polisi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege nchini (TAA), Deusdedit Kato, alisema mtuhumiwa huyo alipokuwa anataka kupita getini, mashine maalum za kukagulia zilibainisha kwamba alikuwa na kitu, na hivyo askari waliokuwapo hapo walimtilia shaka na kumweka pembeni kisha kumkagua na kumkuta na dawa hizo. 

Kato alisema kuwa mpaka sasa bado hawajajua thamani ya dawa hizo ambazo watazipeleka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali ili kupata uthibitisho zaidi iwapo ni dawa za kulevya au la.

Kwa mujibu wa Kato, mtuhumiwa huyo bado anashikiliwa na Polisi na kwamba  muda wowote kuanzia jana walitarajia kumfikisha katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kujibu  mashtaka baada ya kupata majibu kutoka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali.PICHA KWA HISANI YA ITV DAIMA.

 


No comments:

Post a Comment