Wednesday, November 27, 2013

LISSU "ZITTO ANATUMIA JUKWAA PAC KUTUKANYAGA KWA HOJA ZA UONGO"

Baada ya aliyekuwa Naibu katibu Mkuu wa Chadema Zitto Kabwe pamoja na aliyekuwa mjumbe wa kamati kuu wa chama hicho Dr Kitila Mkumbo kuzungumza na waandishi wa habari kuhusiana na hatua ya chama chao kuwavua vyeo vyao vyote ndani ya chama hatimaye Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimewaandikia barua aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu, Zitto Kabwe, na aliyekuwa Mjumbe wa Kamati Kuu, Dk. Kitila Mkumbo, ambao wiki iliyopita walivuliwa nafasi za uongozi, zinazoeleza mashtaka ya makosa 11 wanayotuhumiwa kuyatenda dhidi ya chama hicho.

Mkurugenzi wa Habari na Uenezi wa Chadema, John Mnyika, alisema barua hizo, ambazo Zitto na Dk. Mkumbo, walitarajiwa kukabidhiwa jana, zinawataka wajieleze kwa nini wasichukuliwe hatua zaidi, ikiwamo kufukuzwa uanachama.

Alisema hayo alipozungumza na waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam jana, siku mbili baada ya Zitto na Dk. Mkumbo, kuitisha mkutano na waandishi wa habari, Jumapili wiki iliyopita na kusema hadi siku hiyo walikuwa hawajapata barua hizo zaidi ya kusikia suala hilo kwenye vyombo vya habari.

Mnyika alisema mashtaka ya makosa, ambayo Zitto na Dk. Mkumbo wanatuhumiwa kuyatenda, yanahusiana moja kwa moja na ukiukwaji wa katiba, kanuni, maadili na itifaki ya chama hicho.

Alisema uamuzi wa kuwavua nafasi za uongozi ulifikiwa na Kamati Kuu (CC) ya Chadema katika vikao vyake vilivyofanyika wiki iliyopita.

Mnyika alisema baada ya maamuzi hayo ya CC, juzi sekretarieti yake ilikutana kwa mujibu wa kazi zake za kikatiba.

Alisema ikiwa sehemu ya utekelezaji wa maamuzi ya CC, sekretarieti ilikamilisha mapitio ya yaliyojiri pamoja na maamuzi ya CC juu ya suala hilo pamoja na kukamilisha barua hizo kwa wahusika.

“Na naomba kuwajulisha tu kwamba, leo (jana) wahusika wote (Zitto na Dk. Kitila) watapatiwa barua zao kwa maana kwamba barua zao ziko tayari zinazoeleza maamuzi ya Kamati Kuu,” alisema Mnyika.

Alisema maamuzi ya CC hayakuhusu tu kuwavua uongozi, bali yalihusu vilevile kutakiwa kuandikiwa kujieleza ni kwa nini wasichukuliwe hatua za ziada, ikiwamo kufukuzwa uanachama kutokana na makosa waliyoyafanya na waliyokifanyia chama.

“Na kwa kweli ni makosa waliyoyafanya na ambayo wamekifanyia chama yalielezwa na maamuzi ya Kamati Kuu yaliyotangazwa,” alisema Mnyika.

MAKOSA YANAHUSIANA NA WARAKA

Alisema makosa hayo yalihusiana na waraka ulioandikwa, ambao kimsingi ulikiuka katiba, kanuni, maadili na itifaki ya chama.

“Sasa kwenye mashtaka yao na barua zao ambazo leo watakabidhiwa kumeeleza mashtaka na makosa 11, ambayo watajwa wameyafanya ya kukiuka kanuni, katiba na itifaki ya chama,” alisema Mnyika.

Alisema mashtaka waliyoandikiwa, yamejikita katika maamuzi ya CC, ambayo yalihusu waraka wa siri.

“Na siyo masuala, ambayo wahusika baada ya Kamati Kuu kupitisha maamuzi yale wameyasema kwenye vyombo vya habari masuala ambayo siyo yaliyoifanya Kamati Kuu ifikie maamuzi iliyoyafikia,” alisema Mnyika.

Aliongeza: “Kwa hiyo tayari wahusika wameandikiwa barua na nisisitize kwamba, maamuzi yaliyofanywa na Kamati Kuu ya chama yamefanywa kwa mujibu wa katiba, kanuni, maadili na itifaki ya chama.”

Maamuzi hayo ya CC yalimvua Zitto, ambaye ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini wadhifa za Naibu Katibu Mkuu na kubaki kuwa mwanachama wa kawaida.

Kwa maana hiyo, Zitto ambaye pia alikuwa Mjumbe wa Kamati Kuu (CC) Mjumbe wa Baraza Kuu na Mkutano Mkuu, amebaki kuwa mwanachama wa kawaida.

Aidha, uongozi wa wabunge wa Chadema uliagizwa na CC kumwandikia barua Zitto ya kumwondoa katika nafasi ya Naibu Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni wa Wizara ya Fedha haraka iwezekanavyo kwa tuhuma za kukisaliti chama.

Pia aliyekuwa Mjumbe wa CC, Dk. Kitila, na aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba, ambao nao wamevuliwa nyadhifa zote za uongozi na kubaki kuwa wanachama wa kawaida.

Akijibu yaliyozungumzwa na Zitto na Dk. Kitila baada ya maamuzi ya CC dhidi yao, Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu, alisema ni maneno ya kupoteza lengo kwa kuwa walivuliwa nafasi za uongozi kwa sababu ya waraka ule na siyo kwa sababu ya kile alichokiita uongo wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC).

‘Uongo’ wa PAC unaodaiwa na Lissu, ni kauli iliyowahi kutolewa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Zitto akisema hakuna chama chochote cha siasa, ikiwamo Chadema, ambacho hesabu zake zimekaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Lissu alisema hata Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa inatambua kuwa Chadema ni kati ya vyama, ambavyo hesabu zake zimekaguliwa.

Alisema Chadema ina nyaraka zinazothibitisha hilo tangu mwaka 2010, 2011 na 2012, ambazo Zitto alipokuwa Naibu Katibu Mkuu alipaswa kuzijua.

Lakini alisema Zitto alishindwa kuzijua nyaraka hizo kwa sababu alipokuwa kiongozi wa chama hakuwa na mazoea ya kufika ofisini, badala yake amekuwa akiishia kukitungia uongo chama.

“(Zitto) Anatumia jukwaa la PAC kutukanyaga kwa hoja za uongo,” alisema Lissu.

Mbali na hilo, Lissu alisema pia kuwa Zitto na Dk. Mkumbo hawakuvuliwa nafasi za uongozi katika chama kwa sababu ya yeye (Zitto) kukataa kupokea posho au kuuza majimbo ya uchaguzi, ambayo Chadema ilisimamisha wagombea ubunge katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.

Kuhusu hoja kwamba CC haina mamlaka ya kumvua mwanachama nafasi ya uongozi bali Baraza Kuu la chama, alisema haina msingi kwa kuwa katiba ya Chadema imeipa mamlaka CC kama itaona kuna dharura ya kufanya hivyo.

Alitoa mfano akisema mwaka 2004 aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Amani Kabourou alivuliwa nafasi hiyo na CC. Pia mwaka 2007, CC ilimvua Umakamu Mwenyekiti Taifa, marehemu Chacha Wangwe.

Alisema vipindi vyote hivyo, Zitto alikuwapo na alishuhudia hayo.

“Sasa kama CC ilikuwa sahihi vipindi vyote hivyo basi na sasa ni sahihi,” alisema Lissu.

Alisema mashtaka ya makosa 11, ambayo Zitto na Dk. Kitila wanatuhumiwa kuyatenda hawawezi kuyaweka hadharani, bali watawakabidhi wahusika na kwamba, kama wao wataamua kufanya hivyo hilo litakuwa juu yao.

Hata hivyo, alisema wanaweza kuyaweka hadharani baada ya CC kupokea utetezi kutoka kwa watuhumiwa.

Alisema mwaka 2012, Chadema ilitengeneza mwongozo unaomtaka mwanachama kutangaza kusudio la namna ya kugombea uongozi katika chama na kwamba, walifanya hivyo ili kuzima chokochoko zilizokuwa zimekithiri kuelekea kwenye uchaguzi katika siku za nyuma.

Kwa mujibu wa Lissu, mwongozo huo unataka mwanachama atangaze wazi kusudio lake hilo kwa kupeleka barua kwa Katibu Mkuu na siyo kwa kujificha na kuchafua wengine.

“Kama wangekuwa wanataka mtu wao (awe mwenyekiti wa Chadema) wangetangaza. Maamuzi ya Kamati Kuu ni uthibitisho kwamba hakuna tunayemuogopa,” alisema Lissu.

Alisema ni kweli suala la PAC lilijadiliwa katika vikao vya CC, lakini halikuwa hoja ya kuwashtaki wahusika.
FEDHA ZA SABODO
 

Kuhusu Sh. milioni 100 zilizowahi kutolewa na mfanyabiashara Mustafa Sabodo kwa Chadema mwaka 2009, Lissu alisema zipo kwenye ripoti ya CAG na ile iliyopelekwa na chama kwa Msajili wa Vyama vya Siasa na kwamba, hajawahi kumsikia Zitto akihoji fedha hizo na zile za ruzuku ya chama kwenye vikao vya chama.


No comments:

Post a Comment